AJIZALISHA NA KUTUMBUKIZA MTOTO CHOONI

MSICHANA mmoja mkazi wa Mtaa wa Zaire eneo la Kijenge Kaskazini mkoani Arusha, amelazwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru chini ya ulinzi mkali wa Polisi baada ya kujizalisha mwenyewe na kisha kumtumbukiza mtoto wake kwenye ndoo ya maji.Baba mwenye nyumba ambayo binti huyo alikuwa amepanga chumba cha kuishi, Reuben Mollel alisema msichana huyo alikuwa anajulikana kama 'Dada Pendo,' na kwamba maisha yake hayakuwa wazi.

"Alipokuja kupanga hapa alidai kuwayeye ni mwanafunzi, ila hivi karibuni pia alionekana kuwa na mimba, hakuna kilichojulikana tena hadi jana, ambapo nyumba hii ilizingirwa na wanakijiji ambao hatimaye waligundua kitoto kinachodhaniwa kuwa ni chake, kikiwa kimezamishwa kichwa chini, kwenye ndoo ya maji," alisema baba huyo mwenye nyumba.

Taarifa za uwezekano wa kuwepo mtoto katika chumba cha dada Pendo ziliibuliwa na mpangaji mwenzake, Mama Martha Lucas, ambaye alidai kuwa alisikia sauti ya mtoto mchanga akilia usiku kucha na baadae kutoweka majira ya asubuhi.

Hata hivyo, jirani huyo aliamua kutoa taarifa kwa wapangaji wenzake pamoja na wakazi wenginewa Kimandolu, ambao walimuita Mjumbe wa Mtaa wa Kijenge Kaskazini, Gabriel Joseph na pamoja walianza msako wa kukitafuta kichanga hicho, hii ikiwa ni pamoja na kujaribu kuvunja choo cha shimocha nyumba hiyo, wakidhani kuwa mtoto alitupiwa humo.

Baada ya juhudi zao kuambulia patupu, mkazi mmoja wa eneo hilo,Nelson Kweka, alihisi kuwa pengine chumba cha huyo dada hakikukaguliwa vizuri na ndipo alipofunua mfuniko wa ndoo ya maji ya plastiki na kumkuta mtoto mdogo wa kiume akiwa ametumbukizwa humo, na tayari alikuwa ameshakufa.

Hatimaye polisi walipewa taarifa, lakini mara walipofika kwenye eneola tukio, walimkuta dada mtuhumiwa naye akiwa katika hali mbaya kiafya, pengine kutokana na juhudi za kujizalisha mwenyewe usiku.

Dada Pendo alikimbizwa hospitalini Mount Meru, huku mtoto wake ukipelekwa kuhifadhiwa katika nyumba ya maiti hospitalini hapo.

Ofisa Habari wa Polisi mkoani hapa, Rashid Nchimbi alisema polisi wanasubiri afya ya dada huyo itengemae ili aweze kulisaidia jeshi hilo katika uchunguzi zaidi.

-:Habari Leo