KAMPUNI YA SIGARA KOREA YADAIWA KUFANYA UBAGUZI WA RANGI

Kampuni kubwa ya Tumbako nchini Korea Kusini, imeahidi kubadilisha tangazo lake la kibiashara ambalo limekosolewa kwa kuonekana kuwa la kibaguzi.

Mabango yenye tangazo hilo la aina mpya ya sigara ya kiafrika, yalikuwa na picha za Tumbili waliovalia kama waandishi wa habari wakitangaza kuwa ''Afrika inakuja!" Sigara hizo ni bidhaa mpya ya kampuni ya 'This Africa line'.

Aidha kampuni hiyo inasema kuwa sigara hizo zimetengezwa kwa Tumbako ya kiafrika na ambayo imekaushwa kwa njia za kitamaduni.

Paketi za Sigara zina picha zinazoonyesha Tumbili wakichoma tumbako hiyo.

Kejeli kwa Afrika

"tumeudhiwa sana na picha hii ya kejeli iliyotumiwa na kampuni hiyo ikionyesha Tumbili na kuwahusisha na Afrika,'' alisema, ilisema taarifa ya baraza kwa kudhibiti biashara ya Tumbako ya Afrika ikisema kuwa sharti tangazo hilo liondolewe haraka iwezekanavyo.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa, ''kukejeli Afrika ili kuongeza mauzo ya bidhaa ambazo husababiha vifo na maradhi sio jambo linalokubalikana wala hatutakubali. ''Tangazo hilo la biashara limewekwa katika maeneo ya maduka kote nchini humo.

Hata hivyo msemaji wa kampuni hiyo ameelezea kuwa tangazo hilo litaondolewa madukani mwezi ujao.

Amesema kuwa kampuni imejutia utata uliosababishwa na tangazo hilo na kusema kuwa kampuni hiyo ingependa kuondoa wasiwasi wowowte ulioibuka kutokana na tangazo hilo kuhusu ubaguzi wa rangi Alisema hawakuwa na nia yoyote yakuwa kejeli waafrika na kuwa walichagua kutumia tumbili kwa sababu ni wanyama wazuri wanaowakumbusha watu kuhusu Afrika.

Kampuni hiyo inasema kuwa kwa sababu bidhaa hii ina majani ya tumbako kutoka Afrika, nia ya kampuni ilikuwa tu kufananisha bidhaa hiyo na Afrika.