WATU SABA WA FAMILIA MOJAWAUAWA NAKUCHOMEWA NYUMBA KWA IMANI ZA KISHIRIKINA

Watu saba toka familia nne tofauti  wameuawa na nyumba 18 zimechomwa moto jumanne wiki hii katika kijiji cha murufiti wilaya ya kasulu mkoani kigoma,baada ya wananchi kuvamia wakazi wa nyumba hizo kutokana na imani za kishirikina.

Wakizungumzia tukio hilo ndugu wa watu waliokufa na wakazi wa kijiji hicho wamesema tukio hilo lilitokea usiku , ambapo baada ya tuhuma za ushirikina kushamiri kijijini hapo , wananchi walimualika mganga mmoja ambaye aliainisha watu wanaodaiwa kuwa ni wachawi , hali iliyosababisha wananchi kuzivamia nyumba hizo na kuwaua kwa kuwachoma moto John Mavumba,Elizabert Kaje, Dyaba Kitwe,Vicent Ntiyaba , Herman Ndabiloye, Redamta Mdogo,na Ramadhani kalaliza wote wakiwa na umri wa zaidi ya miaka hamsini na tano huku  wanafamilia wengine wakikimbia hovyo. 
 
Kamanda wa polisi mkoa wa kigoma Jafari Mohamed amesema hadi sasa watu 18 wamekamtwa akiwemo mwenyekiti wa kijiji cha murufiti Evarist Ruhaya na kwamba polisi inaendelea na msako mkali wa kutafuta wengine ambao walihusika na tukio hilo akiwemo mganga wa jadi Faustino Ruchagula ambaye taarifa zinaonyesha alihusika katika masuala ya kupiga Ramli hivyo kuchochea hasira za wauaji. 
 
Matukio ya mauaji kwa imani ya kishirikina yamekuwa yakitokea mara kwa mara mkoani kigoma, ambapo mwaka jana mkazi mmoja wa kijiji cha kibwigwa wilayani Buhigwe aliuawa na na mazao yake kufyeka na watu wasiofahamika.