ANYWA SUMU BAADA YA KUNUSURIKA KUBAKWA

JESHI la Polisi mkoani Tanga linamshikilia mtoto mmoja (16) ambaye ni mkazi wa barabara ya 20 jiijini humo, kwa kosa la kunywasumu kwa lengo la kutaka kujiua, baada ya kunusurika kubakwa na baba yake wa kambo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga,Frasser Kashai alibainisha hayo wakati akitoa taarifa kwa vyombo vya habari kupitia mkutano uliofanyika ofisini kwake jana.

Alisema tukio hilo lilitokea Oktoba 18, mwaka huu nyumbani kwao mtaa wa barabara ya 20 uliopo Kata ya Ngamiani Kusini wakati baba huyo aitwaye Richard Leonard (39) alipokuwa akimvizia ili kutekeleza ubakaji huo.

"Uchunguzi wetu wa awali umebaini kwamba sababu ya chanzo cha mtoto huyo kutaka kunywa sumu ili kujiua ni baada ya kuponea chupuchupu kubakwa na mtuhumiwa ambaye hata hivyo inadaiwa kuwa ni baba yake wa kambo," alisema.

Aidha, aliongeza, "Leonard tayari tumemkamata na huyu mtoto naye kadhalika ingawa kwa sasa yeye amelazwa katika Hospitali ya Mkoa ya Bombo kwa matibabu na taratibu za kuwafikisha mahakamani wote wawili zinaendelea."