ASKARI WA JWTZ APIGWA RISASI NA POLISI

ASKARI wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) MP 104144 Private Lazaro Nassoro amepigwa risasi mguuni na askari wa Jeshi la Polisi baada ya kuleta vurugu baada ya kusimamishwa na askari wa usalama wilayani Tarime mkoani Mara.

Hayo yamebainishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Tarime Kamishna Msaidizi Lazaro Mambosasa wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii jana kwa njia ya simu.

Mambosasa alisema pamoja na private Nassoro, pia askari mwingine wa JWTZ MP 104464 Private Aloyce Engbert alipata majeraha puani na raia mwingine ambaye alikuwa anashuhudia tukio hilo alijeruhiwa.

Kamanda huyo alisema tukio hilo lilitokea baada ya askari huyo wa JWTZ kukiuka sheria na taratibu za barabara ambapo alisimamishwa kwa kosa la kutovaa 'helmet' jambo ambalo liliibua mtafaruku baina yao.

Alisema baada ya askari wa usalama kusimamia sheria askari wa Jeshi la Wananchi aliwasiliana na wenzake hivyo kusababisha mapigano ya ngumi baina ya askari Polisi na wa JWTZ ndipo mmoja wao akapigwa risasi katika kuleta amani.

Kamishna Msaidizi alisema baada ya tukio hilo Jeshi la Polisi liliwashilikia askari hao ambao walipatiwa matibabu na baadae kupelekwa kwenye mamlaka zinazowahusu.

Mambosasa alisema Kamati yaUlinzi imekutana na kuhakikisha kuwa vyombo hivyo vinakuwa na umoja ili kuondoa tafsiri potofu kwa jamii.

Chanzo: Jambo Leo