MWANAMKE ADAIWA KUIBA MTOTO KULINDA NDOA

POLISI mkoani Rukwa wanamshikilia mkazi wa kitongoji cha Chanji, Manispaa ya Sumbawanga, Magreth Juma (34) akituhumiwa kuiba mtoto wa kike mwenye umri wa siku mbili ili asiachike katika ndoa yake, kwa kuwa hajabahatika kumzalia mtoto mumewe.

Hayo yamethibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda ambaye alisema uchunguzi wa awali umeonesha mwanamke huyo, kabla ya kuchukua uamuzi wa kuiba mtoto, alishawahi kuzaa na mwanamume mwingine kabla ya kuwa na mumewe wa sasa.

Hata hivyo, inadaiwa baada ya kuishi na mumewe wa sasa kwa zaidi ya miaka miwili bila kupata mtoto mwingine, alihofia kuvunjika kwa ndoa yake, hasa ikielezwa mumewe alikuwa akidai mtoto.

Mwaruanda alidai kuwa mtuhumiwahuyo alitiwa nguvuni Oktoba 22, mwaka huu asubuhi ikiwa ni muda mfupi tangu mtoto huyo aibwe kutoka kwa mama yake katika kitongoji cha Bangwe.

Aliongeza kuwa awali alfajiri siku hiyo ya tukio, taarifa ziliripotiwa Kituo cha Polisi Sumbawanga na mama mzazi wa mtoto huyo, aitwaye Magreth Benias (28) kuwa mtoto wake mchanga amepotea katika mazingira ya kutatanisha.

“Ndipo polisi kwa kushirikiana na raia wema walianza msako na mudamfupi baadaye walimkamata mtuhumiwa akiwa na mtoto huyo nyumbani kwake...tulibaini kuwa mama wa mtoto huyo na ndugu wa mtuhumiwa waliwahi kuishi nyumba moja ya kupanga ambapo mtuhumiwa alikuwa akifika katika nyumba hiyo kumtembelea ndugu yake,” alieleza.Kamanda Mwaruanda alisema mtoto huyo aliyeibwa, amekabidhiwa kwa mama yake mzazi baada ya kufanyiwa uchunguziwa kitabibu wa afya yake.

Alisema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani baada ya uchunguzi waawali wa shauri lake kukamilika.


Chanzo: Habari Leo