VIKOSI VYA CONGO VYAANZA KUSHAMBULIA FDLR

Vikosi vya Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo FARDC, vimeanzisha hatua za kijeshi dhidi ya waasi wa Rwanda wa kundi la FDLR, Jumanne hiiTangu asubuhi mapema kumeripotia shughuli za kijeshi katika vijiji vya Ruvuye na Mulindi katika misitu ya maeneo ya mji wa Lemera tarafani Uvira mkoani Kivu ya kusini.

Baadhi wa wajumbe wa kundi hilo wanashutumiwa kushiriki katika mauaji ya kimbari ya Rwanda kabla ya kutoroka katika nchi jirani ya Jamuhuri ya kidemokrasi ya Congo,ambako pia wanashutumiwa kutekeleza ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu, yakiwemo mauaji, ubakaji na uporaji.

Mwandishi wa BBC wa mashariki mwa Kongo Byobe Malenga alituandalia taarifa ifuatayo.

Silaha nzito nzito pamoja na bunduki za rashasha zimesikika hii leo tangu asubuhi mapema katika vijiji vya Ruvuye na Mulindi katika misitu ya maeneo ya mji wa Lemera tarafani Uvira mkoani Kivu ya kusini.

Vyanzo vya idara ya 33 ya wanajeshi wa Mkoa zinaonyesha kuwa hatua hio ni alama ya kuanza rasmi shughuli za kijeshi dhidi ya waasi hao wa kihutu toka Rwanda wa FDLR katika mkoa wa Kivu ya Kusini,huku vikisema kua askari wa taifa FARDC,wamedhibiti kambi ya Revo kutoka mikono mwa waasi hao kilomita thalathini na mji wa Lemera.

Kamanda wa harakati hizo maarufu "Sukola 2" dhidi ya wapiganaji wa Rwanda FDLR katika Kivu ya Kusini, Generali Esperant Masudi, yupo kwenye eneo la mapambano katika misitu ya Lemera ajili ya shughuli hizo.

Jeshi la Congo Kupitia Generali Didier Etumba, lilitangaza Januari 29 kama mwanzo wa operesheni dhidi ya waasi wa FDLR.

Lakini mapigano yalikuwa bado kuaanza katika maeneo yote ya hapa nchini.

Raia wa hapa mashariki mwa jamuhuri ya kidemokrasia ya Congo wameonyesha mtazamo wao kuhusiana na hatua hio ya jeshi la Congo FARDC kuanzisha mashambulizi dhidi ya waasi hao.

FDLR wanapatikana sio tu katika mkoa wa Kivu Kusini bali katika maeneo mbalimbali ya ya mashariki mwa hapa nchini kwa zaidi ya miaka ishirini sasa huku wakituhumiwa kwa vitendo vya ualifu.

Hata hivyo, vikosi vya jeshi la DRC FARDC vinaendesha shughuli hizo peke yake, bila msaada wa vikosi vya kulinda amani vya umoja wa mataifa MONUSCO.

Umoja wa Mataifa ulisitisha msaada wake kwa jeshi la Congo kwa kile walichokisema kuwepo wa majenerali wawili ndani ya operesheni hizo ambao wanatuhumiwa kwa ukiukwaji wa haki za binadamu.

Kutokana na utata uliopo katika mawasiliano ya pande hizo mbili,hatua hio ilipelekea serikali ya jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kukataa msaada wowote kutoka kwa vikosi vya umoja wa mataifa MONUSCO katika operesheni hizo dhidi ya waasi wa Rwanda wa FDLR.

Rais Joseph Kabila, alitoa kauli hiyo katika hotuba kwa mabalozi mjini Kinshasa.