JORDAN YALIPIZA KISASI KWA IS

Serikali ya Jordan imewauwa wapiganaji wawili wa kiislamu, waliokuwa wamezuiliwa korokoroni nchini humo na ambao Islamic State ilitaka wabadilishane na rubani aliyechomwa moto pamoja na mwanahabari wa Japan ambaye aliuwawa juma lililopita.

Msemaji wa Serikali Mohammad al-Momani, amesema kuwa waliouwawa ni mlipuaji mmoja wa kike raia wa Iraqi Sajida al-Rishawi na mfuasi wa Al-Qaeda, Ziad al-Karboli.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameungana na mataifa mbalimbali duniani kulaani mauaji ya rubani huyo yaliyofanywa na kikundi cha Islamic State, ambacho pia kinajulikana kama Daesh.

Rubani huyo alikamatwa ndege yake ilipoanguka katika makabiliano na wapiganaji wa IS nchini Syria mwezi disemba.

Jordan ilijaribu kumuokoa luteni Kasasbeh katika ubadilishanaji uliomuhusisha Rishawi.

Alikuwa amehukumiwa kunyongwa kufuatia msururu wa mashambulizi katika mji mkuu wa Jordan Amman ambayo yaliwaua watu 60 mwaka 2005.