BALOTELLI AWATIBUA TENA LIVERPOOL

Nahodha wa timu ya Liverpool Steven Gerrard amemshutumu mchezaji mwenzake Mario Balotelli kwa kuonyesha utovu wanidhamu pale alipolazimisha apige mkwaju wa penalti badala ya Jordan Henderson aliyekuwa tayari anakwenda kupiga adhabu hiyo dhidi ya timu ya Besiktas ya Uturuki.

Balotelli alifunga penalti hiyo na kuiwezesha Liverpool kuibuka washindi wa bao 1-0 katika mchezo wa ligi ya Uropa unaozishirikisha timu 32 uliochezwa Alhamisi katika uwanja wa Anfield.

Hali hiyo ilijitokeza baada ya kushindwa kuelewana na nahodha wa mchezo huo Henderson na Daniel Sturridge juu ya nani abebe jukumu la kupiga penalti hiyo.

Gerrard amesema: "Henderson ni nahodha na Balotelli kwa kiasi fulani alionyesha kumkosea adabu katika hali hiyo."

Gerrard ambaye kwa sasa ni majeruhi, alikuwa mchambuzi katika matangazo ya mchezo huo kwenye televisheni ya ITV ya nchini Uingereza.

Gerrard amesema kuwa Balotelli alikuwa "kwa kiasi fulani kakosea"baada ya mchezaji huyo wa kimataifa wa Italia kumnyang'anya mpira Henderson, ambaye alikuwa amejitayarisha kupiga penalti hiyo.

Henderson alikuwa nahodha wa Liverpool dhidi ya Besiktas, na Gerrard anaamini angekuwepo katika mchezo huo angepiga penalti hiyo.

"Sheria ni sheria," amesema. "Pongezi kwa Mario, amefunga, lakini si vizuri kuona wachezaji wakibishana. Nafikiri Jordan alilichukua suala hilo vizuri."

Kocha wa Liverpool Brendan Rodgers baada ya mchezo huo hakufafanua nani angepiga penalti hiyo.