UMOJA WA MATAIFA WAITUHUMU TANZANIA KWA HALI ILIYOVO DRC

Umoja wa mataifa imezituhumu serikali za Tanzania na Burundi kuhusiana na hali katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.

Ripoti mpya ya kundi la wataalamu wa umoja huo kuhusu Congo, imeituhumu Tanzania kwa kuwaruhusu viongozi wa kundi la waasi wa FDLR kuandaa mikutano nchini humo.

Imeeleza pia kwamba wanajeshi wa Burundi wametekeleza unyanyasaji wa kingono.

Taarifa hiyo ya Umoja wa mataifa inasema kuwa tangu mwaka wa 2013, viongozi wa FDLR na baadhi ya washirika wao wa kisiasa kutoka Ulaya wamekuwa wakikutana nchini Tanzania.

Lakini wachunguzi wa Umoja wa mataifa walipoiuliza serikali ya Tanzania kujibu madai haya ilikanusha kabisa kuwahi kukaribisha mikutano yoyote ya waasi ndani ya ardhi yake na kuongeza kuwa hakujawahi kuwa na mazungumzo yoyote kati ya majeshi yake na wapiganaji wa FDLR.

Umoja wamataifa umesema pia kuwa una ushahidi wa pesa zilizotumwa kutoka taifa hilo la Afrika Mashariki kwa baadhi ya washukiwa nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo.

Ripoti hiyo pia imelaumu kundi hilo la FDLR kwa kutotekeleza ahadi yao ya kusalimisha silaha na kujisalimisha kufikia Januari mwaka huu.

UN inasema kuwa FDLR wamewatuma wazee waliodhoofika kiafya pekee kujisalimisha na kukabidhi silaha chache sana ambazo zina hitilafu.

Kundi la FDLR, liliundwa mwaka wa 2000 na wahutu waliokimbilia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kufuatia mauaji ya kimbari ya Rwanda.

Kundi hilo linapinga utawala wa kitutsi na ushawishi wake katika eneo la maziwa makuu.

Rwanda imekuwa ikitazama kundi hilo kama tisho kubwa kwa utawala uliopo na kwa kauli moja na Umoja wa mataifa imekuwa ikishinikiza kupokonywa silaha kwa wapiganaji wake.

Ripoti hiyo pia imetoa madai ya ubakaji na unyanyasaji wa kimapenzi unaofanywa na wanajeshi wa Burundi katika Kivu ya Kusini.

Wataalamu hao wa Umoja wa mataifa wamependekeza serikali za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo zifanyie uchunguzi madai hayo ambayo wanasisitiza yalifanywa na majeshi ya Burundi pamoja na kikundi cha vijana wapiganaji wajulikanao kama Imbonerakure.