ALBINO MWINGINE ATEKWA

Kumetokea mkasa mwingine kwa mtoto mwenye ulemavu wa ngozi, albino kutekwa katika wilaya ya Chato mkoa wa Geita, kaskazini magharibi mwa nchi hii.

Polisi wameeleza kuwa mtoto huyo aliyetajwa kwa jina la Yohana Bahati mwenye umri wa mwaka mmoja alitekwa nyumbani kwao na watu wasiojulikana jana usiku.

Kwa mujibu wa taarifa za mwandishi kutoka eneo hilo Renatus Masuguliko, polisi wamefika eneo la tukio na kuanza msako mkali dhidi ya watu wanaotuhumiwa kufanya kitendo hicho.

Habari zinasema watu waliokuwa na silaha za jadi waliwaweka chiniya ulinzi Bahati Misalaba na mkewe ambao ni wazazi wa mtoto albino ambaye walimteka na kutoweka naye.

Familia hii pia ina watoto wengine wawili wenye ulemavu wa ngozi, Tabu Bahati mwenye umri wa miaka miwili na Shida Bahati mwenye miaka kumi na mmoja ambao walinusurika kuchukuliwa na watu hao kwa sababu wakati unyama huo ukitendeka nyumbani kwao hawakuwepo walikwenda kucheza kwa majirani zao.

Mama wa mtoto huyo alijeruhiwa vibaya wakati akimpigania mtoto wake asichukuliwe na watu hao.

Matukio ya kuwaua na kuchukua viungo vya albino yaliyasambaa katika mikoa ya kanda ya Ziwa kutokana na imani za kishirikina kuwa viungo vya watu hao vingeweza kuwapatia utajiri na mafanikio mengine katika maishayao, jambo ambalo ni upuuzi mtupu.