ATUPWA JELA MIAKA 30 KWA KUMBAKA MTOTO WA MIAKA 9

Mkazi wa Malampaka mkoani Simiyu, Benedictor Bulobo (30) , ametupwa gerezani atakakotumikia kifungo kwa miaka 30 baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka binti wa miaka tisa.

Alihukumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Maswa juzi na Hakimu Mwandamizi Mfawidhi Agatha Chigulu, baada ya kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka.

Akitoa hukumu hiyo hakimu huyo alisema kuwa anatoa adhabu hiyo ilikukomesha vitendo hivyo na kuwaonya wenye nia mbaya ya kutaka kutenda kosa kama hilo wajifunze na kuacha mwenendo huo.

Chigulu alieleza kuwa kosa hilo ni kinyume na kifungu cha 131 cha sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2012.

Awali mahakama iliambiwa na Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Nassibu Swedy kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo Februari 23 mwaka jana saa 5:00 asubuhi.

Alimnajisi mtoto huyo maeneo ya nyumbani kwake baada ya kumkamata kwa nguvu binti huyo mwanafunzi wa darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Malampaka na kumwingiza chumbani kwake alipombaka.

Alisema mtoto huyo alipata maumivu makali baada ya kuumizwa sehemu za siri, alipiga kelele kuomba msaada na watu walifika katika eneo la tukio, kumkamata na kumfikisha Bulobo katika kituo cha polisi Malampaka.