LIPUMBA AKUBALI TAMKO LA MAASKOFU

Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba ameunga mkono tamko la Jukwaa la Wakristo Tanzania kupinga Katiba Inayopendekezwa, akisema hoja zao ni za msingi kwa kuwa kuna mambo mengi yanayopingwa na wananchi.

Kauli ya Profesa Lipumba ni mwendelezo wa kauli tofauti zilizotolewa na watu mbalimbali kuhusu tamko la jukwaa hilo, wakiwamo wasomi, viongozi wa dini, wanaharakati na wanasiasa kuhusu hatima ya Kura ya Maoni na muswada wa Makahama ya Kadhi.
Alhamisi iliyopita, jukwaa hilo linaloundwa na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT) liliwataka waumini wake kujitokeza kwa wingi kujiandikisha, kushiriki kikamilifu katika elimu ya Kura ya Maoni, na kisha kuipigia kura ya “hapana” Katiba Inayopendekezwa.
Pia, tamko hilo lililotiwa saini na maaskofu Dk Alex Malasusa wa (CCT), Tracisius Ngalalekumtwa (TEC) na Daniel Awet wa CPCT, lilishauri mjadala unaoendelea kati ya Serikali na vikundi vya kidini kuhusu uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi kikatiba na kisheria ufungwe na badala yake ziachiwe taasisi husika za kidini kuamua juu ya masuala hayo bila kuihusisha serikali wala waumini wa dini nyingine.
Jana gazeti hili lilimnukuu makamu mwenyekiti wa TEC, Askofu Severine Niwemugizi akisema tayari tamko hilo limeshasambazwa katika majimbo yote ya kanisa katoliki nchini.
Kauli ya Lipumba
Akizungumzia tamko hilo, Profesa Lipumba alisema ni sahihi kuipinga Katiba hiyo kwa sababu wananchi walilalamikia mchakato wa kupatikana kwa Katiba mpya baada ya kubaini kuwa mambo mengi waliyoyapendekeza yaliondolewa wakati wa Bunge Maalumu la Katiba.
“Wananchi walitaka kuwepo na ukomo wa wabunge wao, viongozi wasifungue akaunti nje ya nchi na mambo mengine yote hayamo kwenye Katiba Inayopendekezwa. Hoja yao (maaskofu) ni ya msingi,” alisema Profesa Lipumba aliyeongoza wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutoka nje ya Bunge la Katiba na kususia mchakato huo moja kwa moja.
Alisema Serikali imeonyesha kutokuwa na uaminifu kwa wananchi ndio maana haikujali hisia zao, badala yake iliamua kuendelea na mchakato huo licha ya baadhi ya wajumbe kuususia.
Profesa Lipumba, ambaye ni mtaalamu wa uchumi, aliongeza kuwa wananchi walitaka kuwepo na utaratibu maalumu kuhusu viongozi wao kupewa zawadi wawapo madarakani, lakini Katiba Inayopendekezwa ililitupa nje suala hilo.
Mahakama ya Kadhi
Kuhusu suala la Mahakama ya Kadhi, Profesa Lipumba alisema pia Serikali isitishe uamuzi wake wa kupeleka Muswada ya Mahakama ya Kadhi katika Bunge lijalo kwa kuwa bado yapo mambo mengi yanayotakiwa kuwekwa sawa.

Profesa Lipumba alisema pamoja na mahakama hiyo kutokuwa ngeni hapa nchini kwa kuwa ilikuwapo Tanzania Bara wakati wa ukoloni na Zanzibar, bado inaendelea kufanya kazi bila tatizo, mfumo unaotaka kutumiwa na Serikali kuianzisha hivi sasa unapingwa na baadhi ya Waislamu na Wakristo hivyo kusababisha mgawanyiko.
Alisema hali hiyo imefikia hapo kutokana na CCM kuliingiza suala hilo kwenye ilani yake ya uchaguzi ya mwaka 2005, hivyo njia bora ya kuondoa sintofahamu iliyopo ni kwa kutumia muda mrefu zaidi katika kutafuta muafaka.
“Ni bora tungetumia muda mrefu zaidi kutafuta muafaka, Serikali isiendelee na muswada huo,” alisema Profesa Lipumba.
Wiki iliyopita, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema Muswada wa Marekebisho ya Sheria mbalimbali, likiwamo suala la Mahakama ya Kadhi, utawasilishwa katika bunge lijalo ukiwa na maudhui ya kuangalia namna ya kuendesha masuala ya imani ya dini ya Kiislamu.
Nyambabe aunga mkono
Katibu mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema anaunga mkono uamuzi uliofikiwa na maaskofu hao kwa kuwa haiwezekani nchi ikapiga Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa wakati wananchi wamegawanyika.
“Msimamo wa maaskofu ni kama wa Ukawa. Bila kuchukua hatua mmomonyoko wa maadili hautaisha,” alisema Nyambabe.
Kuhusu Mahakama ya Kadhi, Nyambabe alisema: “Hakuna mtu anayepinga kuwepo kwa mahakama hiyo, lakini isiwe chini ya serikali moja kwa moja, iwe huru.”
Kauli za wachungaji
Baadhi ya wachungaji waliunga mkono uamuzi wa Jukwaa la Kikristo kwa maelezo kwamba jambo hilo limeamuliwa na viongozi wao wa juu, lazima litekelezwe.
“Kwa kuwa wameshaamua, naamini tutapata hiyo barua haraka tu, lakini mpaka sasa hatujasikia jambo lolote,” alisema Mchungaji Emmanuel Owoya wa Usharika wa Nkwatira, Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Wilaya ya Hai.
Naye, Mchungaji Jackson Mwaisabile wa Kanisa la Pentecostal Assemblies of God (PAG) mkoani Iringa, alisema bado hajauona waraka unaosambazwa na Jukwaa la Maaskofu na kwamba utakapowafikia watajua nini cha kufanya.

Mzee wa Kanisa la Nguvu ya Uponyaji wa Ukombozi (LHPM) la Dar es Salaam, Ayubu Luchenje alisema masuala la Katiba Inayopendekezwa na Mahakama ya Kadhi yanahitaji kuyafahamu vyema kabla mtu hajatoa uamuzi wake.
Luchenje alisema suala la Mahakama ya Kadhi linakiuka misingi ya Taifa kwa kuwa Katiba iliyopo inaitambua nchi isiyo na dini. Alisema kwa msingi huo jambo hilo linafanywa kisiasa kwa malengo ya kutaka kulifurahisha kundi fulani katika jamii.
“Waziri Mkuu Mizengo Pinda anachofanya ni kutaka kuwafurahisha watu fulani tu, jambo hilo haliwezekani ufanye kitu kisichokubaliwa na Katiba,” alisema Luchenje.


CHANZO: MWANANCHI