GWAJIMA ASAKWA NA POLISI KWA KUMKASHIFU PENGO

POLISI Kanda Maalumu ya Dar es Salaam wamefungua jalada la uchunguzi dhidi ya tuhuma za Askofu Josephat Gwajima wa Kanisa la Ufufuo na Uzima za tuhuma za kumkashifu Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam la Kanisa Katoliki, Mwadhamana Polycarp Kardinali Pengo.

Taarifa iliyotolewa jana na Kamandawa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ilisema Askofu huyo anatakiwa kujisalimisha Kituo Kikuu cha Polisi, ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kwa mahojiano.

"Tumepokea malalamiko ya kukashifiwa na kutukanwa hadharani kwa Mwadhama Polycarp Kardinari Pengo ambaye ni kiongoziwa Kanisa Katoliki nchini Tanzania," alidai Kamanda Kova na kuongeza kuwa kashfa na matusi hayo, yamefanyika kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii.

Aidha, alidai kwamba kuna sauti iliyorekodiwa (audio) na picha za video (video clip) zikimuonesha Askofu Gwajima akimkashfu na kumtukana Kardinali Pengo katika hali ambayo pia imewaudhi watu wengine.

Alidai taarifa ya kumtaka Askofu Gwajima ajisalimishe haraka, inatokana na juhudi za kawaida ili kumpata kushindikana.

"Ni muhimu kwa Askofu Josephat Gwajima kuripoti yeye mwenyewe badala ya kutafutwa au kukamatwa ili ajibu tuhuma hizo kutokana na nafasi yake katika jamii," ilisema taarifa ya Kamanda huyo.