AZAM WANUNUA LIGU YA KENYA

Baada ya kuzinunua Lligi Kuu za Tanzania Bara (VPL) na Uganda (UPL), Kampuni ya Azam Media, Jana Ijumaa imenunua rasmi haki za matangazo ya televisheni ya Ligi Kuu ya Shirikisho la Soka la Kenya (FKLPremier League).

Imetangazwa rasmi Jana kuwa Azam TV inayorusha matangazo kwa satelaiti kutoka Tanzania, itakuwa inarusha moja kwa moja 'live' matangazo ya mechiza ligi ya Shirikisho la Soka la Kenya (FKF) baada ya pande zote mbili kusaini makubaliano hayo kwenye Hoteli ya Intercontinental jijini Nairobi, Kenya jana Ijumaa 20 Machi.

Udhamini huo wa miaka mitatu utazifanya mechi za FKF PL zionekana moja kwa moja kwa dau la dola za Marekani mil 2.25 (Kshs mil 2o5.75) ikiwa ni sawa na US$ 750,000 kwa kila msimu.

Imethibitisha na Mwenyekiti wa FKF, Sam Nyamweya, kwamba kila timu inayoshiriki ligi hiyo itapata fungu la Kshs mil 1 kila mwezi huku akitamba kuwa misaada mingi ya kiuchumi inakuja kutoka kwa wadhamini wengine.

Hata hivyo, imeriptiwa na mitandao ya michezo ya Kenya kwamba suala la mgawo wa fedha za klabu bado halijakaa sawa kutokana na kutokamilika kwa mipango ya bajeti ya udhamini.

"Sitaki niseme sana kuhusu ugawo wa klabu, tutajadili kama shirikisho pamoja na wadau na kuangalia bajeti tuliyonayo kabla ya kuliweka wazi suala hilo kwa umma," amesema.

Alipoulizwa kuhusu ruhusa kwa TV za Kenya kujiunga na Azam TV kuonyesha matangazo ya ligi hiyo, Nyamweya alisema suala hilo pia bado linajadiliwa.