AKAMATWA NA VIUNGO VYA BINADAMU NA NYARA ZA SERIKALI

Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi limemkamata na linamshikilia Kulwa Rajabu (35) Mkazi wa Mtaa wa Kashaulili Wilayaya Mpanda kwa tuhuma za kumkamata na viungo vinavyosadikiwa kuwa ni vya Binadamu na nyara za Serikali Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi Kamishina msaidizi mwandamizi Dhahiri Kidavashari mtuhumiwa huyo alikamatwa na viungo hivyo na nyara za Serikali hapo majira ya saa tatu usiku nyumbani kwake katika Mtaa wa Kashaulili mjini hapa.

Alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa kufuatia taarifa ambazo zilikuwa zimelifikia jeshi la Polisi kutoka kwa Raia wema ambao walitowa taarifa kwa polisi kuwa mtuhumiwa ameifadhi viungo vya binadamu na nyara za Serikali ndani ya nyumba yakeg

Alifafanua baada ya taarifa hizo kulifikia jeshi la polisi walianza kufanya uchunguzi kuhusiana na tuhuma hizo zilizokuwa zikimkabili Kulwa Rajabu.

Kamanda Kidavashari alieleza ndipo hapo jana Polisi walipokwenda nyumbani kwa mshitakiwa na walipofika nyumbani kwake walimfanyia upekuzi huku wakiwa na viongozi wa Mtaa huo.

Alisema katika upekuzi huo Polisi walifanikiwa kumkamata mshitakiwa akiwa amehifadhi ndani ya nyumba yake mifupa mitatu ,mshipa mmoja wa chini ya kinena unaodhaniwa ni wa mtu mwanaume na meno mawili viungo hivyo vinadhaniwa ni vya Binadamu

Kidavashari alisema mbali ya mtuhumiwa kukamatwa na viungo hivyo pia mtuhumiwa huyo alikamatwa akiwa amehifadhi ndani ya nyumba yake nyara za Serikali

Alizitaja nyara alizokamatwa nazo mtuhumiwa Kulwa Rajabu kuwa ni kipande cha ngozi ya Kalungu yeye na singa mbili za Tembo.

Kamanda Kidavashari alisema mtuhumiwa anatarajiwa kufikishwa Mahakamani ili akajibu mashitaka mawili ya kupatikana na viungo vinavyosadikiwa kuwa ni vya Binadamu na kupatikana na nyara za Serikali.