KOCHA SYLVESTER MARSH AFARIKI DUNIA

Aliyekuwa kocha Msaidizi wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Sylvester Marsh amefariki dunia Alfajiri ya leo katika hospitali ya Muhimbili alipokuwa amelazwa.

Taarifa zinasema Marsh alikuwa amekuja Muhimbili kuhudhuria kliniki yake ya kawaida juu ya maradhi ya saratani ya koo yanayomsumbua na ghafla hali yake ilibadilika juzi hadi kufariki dunia.

Marsh alianza kuwa Kocha Msaidizi wa timu za vijana Tanzania mwaka 2003 chini ya Alhaj Abdallah Athumani Seif 'King Kibadeni' kabla ya mwaka 2006 kupandishwa timu ya wakubwa, akianza kumsaidia Mbrazil, Marcio Maximo na baadaye Jan Poulsen na Kim Poulsen.

Hata hivyo, baada ya Jamal Malinzi kuingia madarakani Oktoba mwaka juzi, alibadilisha benchi zima la ufundi la Taifa Stars na Marsh akaondoka pamoja na Kim Poulsen.

Tangu hapo Marsh amerudi kufanya kazi katika kituo chake cha Marsh Academy mjini Mwanza, lakini mwaka jana ndipo maradhi ya saratani koo yalipoibuka na akaletwa Muhimbili kwa matibabu.

Mfanyabiashara Abdulfatah Salim, mmiliki wa hoteli ya Sapphire Court, alimsaidia kocha huyo hadi akafanyiwa upasuaji na hali yake kuimarika Februari mwaka jana na kurejea Mwanza.

Marsh alipata ahueni ya kutosha na kuanza tena kazi ya kufundisha watoto wake wa Marsh Academy, kabla ya wiki hii kuletwa Dar es Salaam kuhudhuria kliniki.

Mbali na timu za taifa, Marsh pia amefundisha klabu za Toto Africans ya Mwanza, Kagera Sugar ya Bukoba na Azam FC ya Dar es Salaam.

Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.