Moto wateketeza Bidhaa

Dar es Salaam. Moto mkubwa uliotokana na hitilafu ya umeme, umeteketeza bidhaa za mabilioni zilizokuwa zimehifadhiwa katika maghala ya Kampuni ya Sunda ya jijini Dar es Salaam.
Magari zaidi ya 20 ya vikosi vya zimamoto na uokoaji vya taasisi mbalimbali vilishindwa kuzima moto huo, ulioanza saa 4:45 asubuhi na kuendelea hadi jana mchana.
Akizungumza katika eneo la tukio, Kaimu Kamanda wa Zimamoto Kanda Maalumu, Bakari Mrisho, alisema walichelewa kupata taarifa za moto huo uliokuwa unateketeza maghala hayo ya kuhifadhi vifaa vya ujenzi na samani za ndani la ‘Ubungo Business Park’.
Mmoja wa wamiliki wa maghala hayo ambaye jina lale halikupatikana, alizimia baada ya kuona mali zake zikigeuka jivu.
Baadhi ya vifaa vilivyoelezwa kuwamo kwenye ghala hilo ni pamoja na marumaru, mashine za kufyatulia matofali, jasi, baiskeli, matoroli, mabomba ya plastiki na makasha mbalimbali yaliyokuwa na vocha za simu.
Vifaa vingine ni matairi ya baiskeli, vifaa vya maalumu vya ulinzi (CCTV, Smart Card ) na kontena zipatazo nne za vocha, (Pampasi, chupa za chai, vikombe vya chai vyote  vilitekelea kwa moto huo).
Baadhi ya kampuni zilizokumbwa na janga hilo ni Sandu (T) Limited, Kampuni ya Simu za Mkononi ya Zantel, Poly Machinery na Brick Machinery.
Kaimu Mkurugenzi wa Kampuni ya Sunda (T) Limited, Mashaka Zuberi alisema moto huo ulianza muda mfupi baada ya fundi umeme wa ghala hilo kufanya matengenezo ya kuongeza nguvu ya nishati hiyo.
Alisema fundi wa umeme jana (juzi) alikuwa anafanya matengenezo  ya kuongeza nguvu ya umeme kwani umeme uliokuwapo haukuwa na uwezo wa kuhudumia vifaa vilivyokuwapo.
Zuberi alisema leo (jana) saa 4.30 fundi huyo alifika kumalizia kazi hiyo ambapo aliwataka kuzima vifaa vyote vya umeme ili kuwezesha kuwasha baada ya kumaliza matengenezo.
Naye Kaimu Kamanda wa Zimamoto, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Bakari Mrisho alisema kitendo cha baadhi ya watu kukaidi kuzingatia sheriza zimamoto ndio chanzo cha maafa ya aina hiyo.
Alisema walifanya ukaguzi na kuwataka kuweka kisima cha maji jambo ambalo hawakulitekeleza na kusababisha usumbufu wa kupata maji ya kuzimia moto huo.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Charles Kenyela alisema kutokana na moto huo kuwa mkubwa aliamua kuomba msaada wa magari ya zimamoto kutoka Bandari na Uwanja wa ndege.
Alisema chanzo cha moto huo hakijaweza kujulikana ambapo vitu mbalimbali vimeweza kuteketea kwa moto na hakuna aliyejeruhiwa katika tukio hilo.