MAJAMBAZI YAUA ASKARI MPELELEZI MBEYA

Majambazi yamemuua polisi wa upelelezi, William Mtika (29) wa jijini hapa wakati wa mapambano kwenye tukio la kutaka kupora fedha za Kampuni ya Export And Trading eneo la Iwambi.

Tukio hilo lilitokea juzi saa 9:00 alasiri na katika mapigano hayo, jambazi mmoja alipigwa risasi mguuni na baadaye kufariki dunia kutokana na kuvuja damu nyingi.

Akizungumza wakati wa kuaga mwiliwa marehemu huyo, Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Ahmed Msangi alisema Mtika akiwa na askari wenzake walipata taarifa za watu waliotiliwa shaka nyendo zao eneo hilo ndipo wakaelekea kwenye tukio.

"Askari wakiwa eneo la tukio walifanikiwa kuwakamata majambazi waliokuwa kwenye pikipiki baada ya kugonga gari la Polisi kabla ya nyingine kutokea na kuwapiga risasi ambazo moja ilimpata askari wetu Mtika," alisema.

Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Nyerembe Mnasa aliwataka polisi kutorudi nyuma katika mapambano, huku akiwasisitiza wananchi kutoa taarifa za watu wanaowatilia shaka katika maeneo yao.

Mwili wa marehemu Mtika uliagwa jana mchana nyumbani kwake eneola Ghana Mbeya na kusafirishwa kwenda mkoani Mara kwa ajili ya mazishi.

Alisema polisi pia walifanikiwa kukamata bastola moja iliyotengenezwa kienyeji inayotumia risasi za Shotgun na pikipiki mbili.

Akifafanua chanzo cha tukio alisema, awali majambazi walimvamia mfanyakazi wa kampuni aitwaye Madhu Basavaranjappa lakini alipiga risasi juu ambazo ziliwafanya nao wajibu na hatimaye kuamua kukimbia na ndipo walipokutana na polisi.

Kamanda Msangi alisema wanaendelea na msako mkali wa kuwatia nguvuni majambazi hao huku akisisitiza kwamba kifo cha polisi wake katu hakitawavunja moyo polisi bali kitaongeza morali kuhakikisha wanapambana na aina yoyote ya uhalifu.

Chanzo: Mwananchi