LIPUMBA KUCHUKUA FOMU YA URAIS

Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba (pichani), Jumapili anatarajiwa kuchukua fomu ya kugombea urais.

Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi wa CUF, Shaweji Mketo, alisema jana kuwa mchakato wa kutangaza nia ya kugombea urais ulianza Mei 10 hadi Juni 10, mwaka huu na kuwa hadi kufikia jana ambayo ilikuwa siku ya mwisho walikuwa wamepokea jina Lipumba pekee.

"Mchakato wa utangazaji nia ya kugombea ndani ya chama ulifunguliwa Mei 10 na hadi kufikia jana, tumepokea jina la Prof. Lipumba tu katika ngazi ya urais," alisema.

Aidha, alisema walipanga wagombea waliotangaza nia ya kugombea urais kuchukua fomu kuanzia Juni 11, mwaka huu, lakini kwa kuwa mgombea mmoja ndiye amejitokeza wakapanga Juni 14, 2015 iwe siku ya mwisho kuchukua fomu kwa ngazi hiyo.

Alisitiza kuwa wananchama na wananchi wanatakiwa kujitokeza kwa wingi kwenda kumsikiliza Prof. Lipumba ambaye ataeleza kwa nini amechukua fomu kugombea urais.

Aliongeza kuwa Baraza la Kuu la Uongozi la chama hicho linatarajiwa kukutana Julai 11 na 12, mwaka huukwa ajili ya uteuzi wa mwisho wa wagombea katika ngazi ya ubunge na urais na kuwa hadi Julai 20, mwaka huu vyama vyote vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vimekubaliana viwe vimemaliza kuteua wagombea ambao watapitishwa katika vikao vya Ukawa.

Mketo alisema katika majimbo 189 ya Tanzania Bara, tayari wameshapata wagombea waliotangaza nia ya kugombea kwenye majimbo 133 wakati 56 bado hayajatangaziwa nia.

CHANZO: NIPASHE