AUAWA KWA KIPIGO JWA KUPINGA MAMA YAKE KUOLEWA NA KIJANA

MKAZI wa kitongoji cha Izia, manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa, Sylvester Mtoni (32) ameuawa kikatili na baba yake wa kambo wakishirikiana na bibi yake baada ya kushambulia kwa ngumi, mateke na rungu.

Mtafaruku huo ulitokea baada ya marehemu kuamua kumfukuza baba yake huyo wa kambo anayefahamika kwa jina moja la Bea mwenye umri wa miaka 32 akipinga uamuzi wa mama yake mzazi kuishi nae kinyumba katika nyumba aliyoijenga marehemu baba yake.

Inaelezwa kuwa wakati mkasa huo ukitokea mama mzazi wa marehemu alikuwa safarini akielekea jijini Dar es Salaam.

Inadaiwa kuwa mtoto huyo alimkatalia mwanamume huyo kumwoa mama yake mzazi kwa kuwa ni kijana mwenzake umri wao ukilingana ambao ni nusu ya umri wa mama yake mzazi.

Akithibitisha kutokea kwa mkasa huo Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoawa Rukwa, Leonce Rwegasira alidai kuwa ulitokea juzi usiku katika kitongoji cha Izia Manispaa ya Sumbawanga.

Alieleza kuwa chanzo chake ni kuwa marehemu alipinga uamuzi wa mama yake mzazi kuolewa na mwanaume ambaye ana umri sawa na yeye (Sylivester) na kuishi katika nyumba aliyoijenga marehemu baba yake.

"Usiku huo wa tukio mtuhumiwa ambaye anatafutwa na jeshi la polisi alimshambulia mwanawe huyo wa kambo akisaidiwa na mama mkwe wake wakimpiga kwa ngumi matekena kipande cha ubao hadi kijana huyo alipopoteza fahamu," alieleza Kaimu Kamanda Rwegasira.

Akifafanua aliongeza kuwa alikimbizwa Hospitali ya Mkoa ambapo alikufa akiwa anaendelea na matibabu hospitalini hapo.