KIJANA JELA MIAKA 30 KWA KUMLAWITI MWANAFUNZI

MAHAKAMA ya Wilaya ya Tabora imehukumu Masudi Nassor (20) kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na hatia ya kumlawiti mwanafunzi wa kike wa shule ya msingi mwenye umri wa miaka tisa.

Akitoa hukumu hiyo jana Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Bahati Chitepo alisema kwamba ametoa adhabu hiyo ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye nia kama hiyo kama kijana huyo mdogo.

Alisema kitendo alichofanya kijana huyo mwenye nguvu ya kufanya kazi na kupata mwenzi wake wanayelingana umri inaonesha wazialifanya hivyo makusudi.

Hata hivyo Hakimu Chitepo alisema kwamba ushahidi uliotolewa mbele ya Mahakama hiyo kutoka kwa mganga aliyemhudumia mtoto huyo katika Hospitali ya Kitete unaonesha wazi kwamba mshtakiwa alimwingilia mtoto huyo kinyume na maumbile yake na kumsababishia maumivu makali.

Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo Mwendesha Mashitaka wa Serikali aliiomba Mahakama hiyo itoe adhabu kali kwa mshitakiwa huyo kwa kile alichoeleza kuwa hilo ni kosa lake la pili hivyo adhabu hiyo itakuwa fundisho kwa watu wengine wenye nia mbaya.

Awali Mwendesha Mashitaka alieleza Mahakama hiyo kwamba mnamo Januari 22, mwaka huu majira ya asubuhi katika Kata ya Kiloleni, Manispaa ya Tabora, Nassor akiwa anaendesha baiskeli alikutana na mlalamikaji akiwa anakwenda shuleni na kuomba lifti.

Baada ya kumpandisha kwenye baiskeli Nassoro alikwenda naye kwenye pori la Kalunde ambapo alimlawiti mara tatu na kumtelekeza huko kisha kukimbia lakini alikamatwa na askari Jeshi aliyekuwa dori katika kambi hiyo nakumfikisha Polisi.

Hata hivyo mshitakiwa huyo aliiomba Mahakama hiyo impunguzie adhabu kwani anaishi na babu yake mlemavu wa mguu na wazazi wake wote wamefariki.