MWALIMU KORTINI KWA KUMLAWITI MWANAFUNZI

Makamu Mkuu wa Shule ya Sekondari Usevya wilayani ya Mlele, Makonda Ng-onga amefikishwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Mpanda kujibu tuhuma za kumlawiti mwanafunzi wake anayesoma kidato cha tano.

Mtuhumiwa  alifikishwa kizimbani hapo juzi na kusomewa mashtaka hayo na mwanasheria wa Serikali, Gregory Mhangwa mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Chiganga  Ntengwa.

Mhangwa alidai mahakamani hapo kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo kwa nyakati tofauti katika kipindi cha Novemba  mwaka jana hadi Aprili mwaka huu katika maeneo ya shule hiyo.

Alidai mtuhumiwa alitenda kosa  hilo kwa kutumia nafasi yake ya mkuu wa shule msaidizi, jambo ambalo ni kosa kinyume na kifungu  cha  sheria Na. 154 kifungu kidogo sura ya 16 ya sheria iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Mwalimu huyo anadaiwa kutenda  kosa hilo baada ya kuwa mwanafunzi anapokuwa  amefanya kosa shuleni hapo, humlazimisha kumwingilia kinyume cha maumbile kama adhabu, na endapo  mwanafunzi   atakataa amekuwa akimtishia kumfukuza shule .
Mwalimu huyo ambaye alikana mashtaka hayo, yupo nje kwa dhamana baada ya kutimiza masharti yaliyomtaka kulipa Sh 3milioni mahakamani.

Hakimu  Chiganga aliharisha  kesi  hiyo  hadi Juni 27, mwaka huu itakapotajwa tena.