AJALI YA BUS NA TRENI YAUWA WATU WANNE

Watu wanne wamefariki papo hapo na wengine zaidi ya arobaini kujeruhiwa baada ya Treini ya mizigo,kuligonga basi kampuni ya Don't Worry lililokuwa likitokea mjini Tabora kuelekea ufuruma uyui mkoani humo lilipofika eneo la kuvuko cha reli eneo loa malolo manispaa ya Tabora katika kile kilichodaiwa kuwa ni uzembe wa dereva.

Mashuhuda wa ajali hiyo wamesema kuwa, dereva aliyekuwa katika mwendo wa kasi alitaka kukatiza haraka bila kuzingatia eneo hilo inapopita Treini hata kama aliiona Treini hiyo, na ndipo alipokata kona ya ghafla na basi hilo kuanguka kwenye reli na Treini kuigonga na kukutoa paa lote la juu la gari.

Aidha kaimu kamanda wa polisi mkoani Tabora kamishina msaidizi Juma Bwire amesema kuwa katika ajali hiyo ya basi lenye namba za usajili T568 ABP,wanaume watatu na mwanamke mmoja wamepoteza maisha huku dereva aliyejulikana kwa jina la Kaonjo Iddy (34) akitoroka baada ya kusababisha ajali hiyo ambapo majeruhu wamepelekwa katika hospitali ya rufaa na mkoa wa Tabora.

Viongozi wa shirika la reli waliofika katika eneo la ajali hiyo wamesema kuwa madereva hawazingatii usalama wa barabarani kwani shirika la reli limejitahidi kuhakikisha linaweka alama husika lakini kutokana na mazoea mabaya hawajali na matokeo ni kusababisha ajali mbaya kama hiyo.

BULAYA AIKACHA CCM

Hali imeendelea kuwa tete ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum CCM mkoa wa Mara, Ester Bulaya, kutangaza kukitosa kwa kutangaza uamuzi wake wa kutogombea ubunge kwa tiketi ya chama hicho.

Bulaya ambaye alikuwa mbunge machachari kabla ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuvunjwa na Rais Jakaya Kikwete, hivi karibuni , ametangaza kutogombea ubunge kupitia CCM wakati akizungumza na NIPASHE baada ya kazi ya kuchukua fomu ndani ya chama hicho na kurejesha kuhitimishwa rasmi nchini jana.

Tangu mwanzo mwa mwaka huu, Bulaya alitangaza kugombea ubungekatika Jimbo la Bunda kupambana na Mbunge aliyemaliza muda wake ambaye ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira.

Bulaya amekuwa kada wa pili ambaye alikuwa mbunge kutangaza kutogombea ubunge kwa tiketi ya CCM, mbunge wa kwanza kutangaza kutogombea ubunge kupitia CCM baada ya James Lembeli, ambaye alikuwa Mbunge wa Kahama.

Hata hivyo, Bulaya hakuweka wazi kama ana mpango wa kuhamia chama kingine cha siasa na kutimizaazma yake ya kuwania ubunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Ingawa Bulaya hajaweka wazi, vyama ambavyo vimekuwa vikitajwakusubiri makada kutoka CCM kujiunga navyo ili wawanie ubunge ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ACT-Wazalendo na Chama cha Wananchi (Cuf).

M/KITI MONDULI APIGILIA MSUMARI
Wakati ikiwa hivyo kwa Bulaya, hali bado si shwari ndani ya CCM Wilaya ya Monduli baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Monduli, Edward Sapunyo, Kupigilia msumari wa mwisho na kubariki hatua ya madiwani wake 20 kukihama chama hicho na kujiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Akizungumza mjini hapa jana, Sapunyo ambaye alikuwa Diwani wakata ya Moita, alisema madiwani wake hawawezi kusubiri hadi Mbunge wa Jimbo la Monduli na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, atoe kauli kuhusu hatma yake ya kisiasa ndani ya CCM.

Kauli ya Sapunyo ambaye hatagombea udiwani uchaguzi wa mwaka huu, imekuja siku moja baada ya madiwani 20 wa jimbo hilo kutangaza rasmi kukihama chama hicho na kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

"Hatuwezi kuona baba yetu anapigwa na kuanguka chini halafu tusubiri kauli yake, ni lazima tuchukue hatua mara moja…hii haivumiliki, kitendo alichofanyiwa (Lowassa) na vikao vya CCM mjini Dodoma hivi karibuni kwa kukata jina lake pasipo kumpa haki ya kumsikiliza siyo cha kidemokrasia," alisema.

Lowassa na makada wenzake wa CCM 38 walichukua fomu ya kuomba ridhaa ya kuteuliwa na chama hicho kupeperusha bendera ya kuwania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.

Katika kinyanyang'anyiro hicho, jina la Lowassa na wenzake yalikatwa katika hatua ya mwanzo, hali ambayo imezua malalamiko kwamba ikidaiwa kuwa hawakupewanafasi ya kuhojiwa.

"Tumepigwa, tumesambaratika (CCM) Monduli, hatuwezi kuchukua fomu za kuomba kugombea au kutetea nafasi zetu ndani ya chama hiki, tumehamia Chadema," alisema.

Akizungumzia hali ilivyo, Katibu wa CCM Wilaya ya Monduli, Elisante Kimaro, alidai kuwa siyo kweli kwamba madiwani wote wamekihama chama chao.

Kimaro alidai kuwa baadhi ya madiwani waliotangaza kukihama chama hicho wameanza kusalitiana.

Alisema madiwani hao ambao anawaita ni makada baada ya Barazala Madiwani la Halmashauri ya Monduli kuvunjwa, walifanya mkutano kwa kushawishiwa na mmoja wao.

Alisema ushawishi huo unatokana na uchu wa madaraka alionao kwa kuwa tayari wananchi wa Jimbo la Monduli, wanapenda aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum CCM, Namelok Sokoine, kuchukua fomu za ubunge wa jimbo hilo.

Alisema kutokana na ugumu huo, diwani huyo wa zamani ametumia mbinu ya kuwarubuni wenzake wakihame chama hicho ili agombea ubunge kwa tiketi ya Chadema.

"Huo ni uchu wa madaraka aliyo nayo," alisema na kuongeza: "Diwani huyo hakubaliki na wananchi wa kata yake."Alidai kabla ya kutangaza kukihakama chama hicho, madiwanihao walikuwa wameshafanya kikao na kuweka azimio la pamoja la kuondoka CCM, lakini juzi walipotangaza uamuzi wao, walijikuta wapo madiwani watatu.

Alisema baadhi ya madiwani walimfuata ofisini kwa lengo la kumuomba radhi lakini yeye aliwaambia waende kuwaomba radhi wananchi katika kata zao.

"Madiwani wachache walikuja hapa ofisini kuomba radhi kwa Katibu wa CCM Wilaya, nikawaambia waende kuwaomba radhi wananchi," alisema.

Akimzungumzia Lowassa, alisema anachoelewa ni kwamba hajatoa tamko lolote kama anakihama chama hicho kama inavyodaiwa na baadhi ya watu na mitandao ya kijamii.

"Bado tuna imani na Lowassa kuwa ni CCM, mpaka sasa hajatoa tamko lolote kukihama chama, lakini ikiwa vinginevyo itakuwa hatari kubwa," alisema.

Imeandikwa na Thobias Mwanakatwe, Salome Kitomari, Dar, George Marato, Musoma na John Ngunge, Arusha.


CHANZO: NIPASHE

PINDA AUTOSA UBUNGE

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, amekataa ombi la wakazi wa jimbo lake la uchaguzi la Katavi la kumtaka agombee tena ubunge katika jimbo hilo ili kuendeleza mipango ya maendeleo aliyoianzisha.

Taarifa iliyotolewa jana kwa vyombovya habari ilimnukuu Pinda akijibu maombi ya wakazi hao baada ya Ibada ya Jumapili iliyofanyika katika Kigango cha Kanisa Katoliki cha Kibaoni Wilaya ya Mlele mkoani Katavi.

Pinda alisema anamshukuru Mungu kwa nafasi aliyopewa ya kulitumikia Taifa akiwa Waziri Mkuu kwa miaka minane na anaamini wakati umefikawa yeye kuwaachia wengine nafasi ya ubunge wa Jimbo la Katavi.

Alisema ataendelea kuwa karibu na wakazi wa jimbo hilo wakati wote nakwa vile atakuwa na muda wa kutosha kushiriki kikamilifu katika mikakati ya kuwaletea maendeleo ili wajikwamue kutoka kwenye umaskini.

Kwa upande mwingine, Pinda aliwaasa wakazi wa jimbo hilo wawemakini kuchagua mbunge na madiwani na kamwe watoa rushwa na wabadhirifu wasipewe nafasi katika uchaguzi ujao utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu.

Akimshukuru Waziri Mkuu, Paroko wa Parokia ya Usevya wilayani humo, Padri Aloyce Nchimbi, aliwaasa wakazi wa Mlele kumuenzi Pinda hata atakapokuwa amestaafu kwani bado watahitaji busara na uzoefu wake katika kujiletea maendeleo.

Pinda yuko kijijini kwake Kibaoni ajili ya mapumziko mafupi na alitoa msimamo wake huo jana ikiwa ni siku ya mwisho kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutoa na kupokea fomu kwa makada wake wanaoomba wateuliwe kugombea ubunge na udiwani katika uchaguzi huo utakao vishirikisha pia vyama vya upinzani.

Msimamo huo wa Pinda umekuja siku chache baada ya jina lake kukatwa katika kinyang'anyiro cha urais ndani ya CCM hivi karibuni mjini Dodoma.

Pinda alikuwa kati ya wanachama 38wa CCM waliojitosa katika kinyang'anyiro cha urais kwa tiketi ya chama hicho.

Hata hivyo, jina lake lilikuwa miongoni mwa majina yaliyokatwa kwa mara ya kwanza na kubakia matano ambayo yalipelekwa kwenye Kamati Kuu (CC) ya CCM.

Majina yaliyopelekwa kwenye kamati hiyo yalikuwa ni ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, Dk. Asha-Rose Migiro, Balozi Amina Said Salum na January Makamba.

Majina hayo yalipelekwa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM ambapo wajumbe wake walipitisha majina matatu kati ya matano.

Waliopenya katika kinyang'anyito hicho ni Dk. Magufuli, Dk. Migiro na Amina na kupelekwa mbele ya Mkutano Mkuu na wajumbe kupiga kura na kumpata Dk. Magufuli atakayepeperusha bendera ya chama hicho kumtafuta Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pinda aliteuliwa kushika wadhifa wa Uwaziri Mkuu na Rais Jakaya Kikwete, baada ya aliyekuwa akishikilia wadhifa huo, Edward Lowassa, kujiuzulu baada ya kuhusishwa na kashfa ya Richmond mwaka 2007.

BODI YA MIKOPO KWA WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU YAONGEZA MUDA WA MAOMBI HADI JULY 31

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeongeza muda wa waombaji mikopo kwa mwaka wa masomo 2015/2016 kuwasilisha maombi yao hadi mwishoni mwa mwezi huu (31 Julai, 2015).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo (Jumatano, Julai 15, 2015) na Mkurugenzi Mtendaji wa (HESLB) Bw. George Nyatega, hatua hiyo imechukuliwa ilikuwapa fursa wombaji ambao hawajakamilisha kufanya hivyo.

"Hatua hii imechukuliwa ili kuwapa fursa wale ambao kwa sababu mbalimbali hawakuweza kufanya maombi ya mikopo katika muda uliopangwa," amesema Bw. Nyatega katika taarifa yake iliyosambazwa kwenye vyombo vya habari.

Itakumbukwa kuwa awali Bodi ilianza kupokea maombi kwa njia ya mtandao (www.olas.heslb.go.tz) tarehe 4 Mei, 2015 na mwisho wa kuwasilisha maombi ulipangwa kuwa tarehe 30 Juni, 2015.

Kupitia taarifa yake, HESLB imewataka waombaji wa mikopo kwa mwaka wa masomo 2015/2016 ambao hawajakamilisha maombi yao kukamilisha na kuwasilisha maombi yao ya mikopo ndani ya muda ulioongezwa na kusisitiza kuwa hakutakuwa na muda mwingine wa nyongeza baada ya tarehe 31 Julai, 2015.

HESLB ilianzishwa kwa sheria ya Bunge na 9 ya mwaka 2004 na kuanza kazi rasmi mwezi Julai, 2005 ili, pamoja na majukumu mengine kutoa mikopo kwa wanafunzi wahitaji waliodahiliwa katika taasisi za elimu ya juu.

MAGUFULI NDIYE MGOMBEA WA URAIS CCM

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimemtangaza daktari John Magufuli kuwa mgombea wake wa kiti cha Urais katika uchaguzi mkuu wa ujao.

Daktari John Magufuli, alisajili asilimia 87.1 % ya kura za wajumbe, hiyo ikiwa ni kura 2104.

Bi Amina Salulm Ali alimaliza katika nafasi ya pili akiwa na asilimia 10.5 % ya kura zote ikiwa ni sawa na kura 253.

Dk. Asha-Rose Migiro akijizolea asimilia tatu ya kura ya wajumbe ama kura 59(2.4%).

Kufuatia ushindi huo Daktari Magufuli ndiye atakaye kuwa mgombea urais wa chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu

Mpaka sasa haijafahamika nani atakuwa mgombea mwenza.

Hata hivyo tetesi zilizoenea zinaashiria kuwa Amina Salum Aliana nafasi kubwa ya kuchaguliwa kuwa mgombea mwenza kutokana na kwamba yeye ndio amekuwa wa pili katika kinyang'anyiro hicho.

Pia ikizingatiwa kwamba yeye ni mtanzania mwenye asili ya Zanzibar.

WAZIRI MKUU WA SERBIA APIGWA MAWE BOSNIA

Waziri mkuu wa Serbia Aleksandar Vucic,amepigwa mawe na kufukuzwa na raia wa Bosnia katika hafla ya ukumbusho wa miaka 20 ya mauaji ya halaiki ya watu katika mji wa Srebrenica Waziri huyo alilazimika kutorokea maisha yake bada ya kutupiwa chupa mawe na matusi.

Mashamblizi hayo yalitokea bwana Vucic alipokuwa akiondoka kwenye hafla hiyo iliyoandaliwa katika makaburi ya takriban wahanga 136 wa mauaji hayo.

Inaaminika kuwa waziri Vucic aligongwa na jiwe kichwani.

Vikosi vya majeshi ya Bosnia Serbia viliwaua wanaume 8000 waisilamu na wavulana wa Srebrenica baada ya kuvamia kambi ambayo ilistahili kulindwa na umoja wa mataifa.

Mauaji hayo yanadaiwa kuwa ndiyo yaliyoisababisha Yugoslavia kuvunjika.

Hii leo sherehe hizo zitakamilika kwa maziko ya waathiriwa136 ambao mabaki yao yalitambuliwa hivi majuzi kwa kutumia DNA.

Rais wa zamani wa marekani Bill Clinton ni mmoja wa wale wanaodhuruia maadhimisho hayo.

Awali waziri mkuu Vucic alikuwa ametoa risala za rambirambi japo aliepuka kukiri kuwa yalikuwa mauaji ya halaiki.